Maandamano zaidi kufanyika Misri leo

...................



Wafuasi wa rais wa zamani wa Misri Mohamed Morsi
Wafuasi na wapinzani wa rais wa Misri aliyeondolewa madarakani Mohamed Morsi wanajiandaa kwa maandamano makubwa mjini Cairo, huku waumini wa dini ya Kiislamu wakiadhimisha Ijumaa ya kwanza ya mwezi mtukufu wa Ramadan.
Wafuasi wa Bwana Morsi wanatarajia kuwa mamilioni ya raia wa nchi hiyo, wataendelea kuunga mkono wito wao wa kutaka Bwana Morsi kurejeshwa madarakani.
Wapinzani wa rais huyo wa zamani ambao waliandamana hadi rais huyo akaondolewa madarakani na jeshi watakusanyika katika medani ya Tahrir.
Watu kadhaa wameuawa kwenye ghasia zilizotokea tangu Morsi alipoondolewa.
Mwandishi wa BBC mjini Cairo, Jim Muir anasema vuguvugu la Muslim Brotherhood huenda liliwatenga raia wengi wakati wa utawala wa Morsi, lakini bado raia wengi wa nchi hiyo hawataki jeshi kuingilia masuala ya siasa.

Marekani kutuma ndege za kivita Misri

Siku ya Alhamisi serikali ya Marekani, ilitoa wito kwa utawala mpya wa Misri, kusitisha harakati zake za kuwakamata wanachama wa vuguvugu la Muslim Brotherhood na kuonya dhidi ya kulenga kundi lolote.

Wanajeshi wakishika doria mjini Cairo
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon vile vile ameonya utawala huo wa Misri kutotenga chama chochote cha kisiasa katika harakati za kutatua mzozo wa kisiasa unaokumba taifa hilo.
Hata hivyo msemaji wa Ikulu ya White House, Jay Carney amesema, utawala wa Washington hauamini kuwa ni lazima isitishe misaada yake ya Misri.
Marekani inatarajiwa kupeleka ndege nne za kivita aina ya F-16 nchini Misri, lakini haijathibitisha kuwa msaada huo utatolewa lini.
Serikali ya Marekani imesema, inachunguza ikiwa aumuzi huo wa jeshi la Misri kumuondoa madarakani rais Morsi ni mapinduzi ya Kijeshi kwa kuwa sheria za Marekani inazuia serikali kutoa misaada kwa nchi yoyote ambayo kiongozi aliyechaguliwa kwa njia ya kidemokrasia ataondolewa kupitia mapinduzi.
Wafuasi wa rais Morsi wamekuwa wakiandamana wiki nzima karibu na kambi ya kijeshi iliyoko Mashariki mwa mji mkuu wa Cairo, ambako wanaamini kuwa kiongozi wao anazuiliwa na maafisa wa kijeshi tangu alipoondolewa madarakani.


Wakati,Jeshi latoa onyo kali kwa waandamanaji Misri


Jeshi la Misri limetoa onyo kali, kwa yeyote ambaye ana nia ya kuvuruga usalama na uthabiti wa taifa hilo wakati huu nchi hiyo unakumbwa na mzozo wa kisiasa.
Waziri wa Ulinzi Abdel Fatah al-Sisi amesema hatma ya taifa hilo siku sijazo ni muhimu sana na kamwe hawataruhusu vurugu au uchochezi wa aina yoyote.
Tangazo hilo limetolewa wiki moja tu, baada ya jeshi la nchi hiyo kumuondoa madarakani rais Mohamed Morsi na kumteua jaji mkuu Adly Mansour kuwa kaimu kiongozi wa taifa hilo.
Wafuasi wa rais Morsi wamekuwa wakiandamana tangu rais huyo alipoondolewa madarakani.
Awali, maafisa wakuu wa chama cha Muslim Brotherhood, wamepinga vikali pendekezo la rais wa mpito Adly Mansour kuweka ratiba ya kuandaa uchaguzi mkuu mwaka ujao.
Wanajeshi wa Misri wakishika doria
Mmoja wa viongozi wa chama hicho, Essam al-Erian anasema kuwa mpango huo utakaojumuisha mabadiliko ya kikatiba na kura mwaka ujao unarejesha nchi hiyo ilipokuwa baada ya mapinduzi ya kumwondoa mamlakani Hosni Mubarak.
Rais wa mpito alitangaza kuwa uchaguzi utafanyika mwaka ujao katika juhudi zake za kutuliza maandamano na hali ya taharuki nchini humo.
Tangazo hilo lilitolewa wakati mgogoro ukizidi kati ya jeshi na wafuasi wa rais aliyepinduliwa Mohammed Morsi karibu na kambi ya jeshi mjini Cairo ambako zaidi ya watu 50 waliuawa hapo jana wakati wa mapigano na wanajeshi.
Aidha tangazo la Rais Adly Mansour, linaashiria mageuzi katika katiba kwa kuitisha kura ya maoni ambayo huenda ikachangia kufanyika kwa uchaguzi mwaka ujao.

Watu zaidi wauawa

Hii inakuja wakati ambapo watu 51 wamethibitishwa kuuawa mjini Cairo.
Waandamanaji wakikabiliana na Jeshi nchini Misri
Chama cha Muslim Brotherhood kinasema kuwa wanachama wake walipigwa risasi wakati walipokuwa wanakesha nje ya makano ambapo Morsi anazuiliwa, lakini jeshi linasema liliwafyatulia risasi kwani waandamanaji nao walikuwa wamejihami.
Rais Morsi, aliyekuwa rais wa kiisilamu na wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia, aliondolewa mamlakani na jeshi wiki jana baada ya maandamano makubwa ya kumpinga kufanyika.
Wafuasi wake wanatuhumu jeshi kwa kufanya mapinduzi, lakini wapinzani wake wanasema hatua hiyo ni mwendelezo wa mapinduzi yaliyomwondoa mamlakani aliyekuwa rais Hosni Mubarak mwaka 2011.
Amri hiyo inasema kuwa jopo la kufanyia katiba marekebisho ambalo lilifutwa kazi wiki jana, litaundwa tena katika kipindi cha siku 15.
Mabadiliko hayo kisha yatapigiwa kura ya maoni. Mchakato utapangwa kufanyika katika muda wa miezi minne.
Baada ya kura ya maoni , uchaguzi wa wabunge huenda ukafanyika mapema mwaka 2014.
Hatimaye uchaguzi utafanyika punde baada ya bunge jipya kuundwa.

chanzo:bbcswahili
http://3.bp.blogspot.com/-e0QpO-QtZzE/U5DWDUZasXI/AAAAAAAABWg/QlFF97gwNdc/s1600/RAHA+GIF.gif
GIVE YOUR OPINIONS HERE

0 comments: